http://tropicalpoultryfarming.blogspot.com/

Mourinho atekwa na hisia akipokea tuzo


Jose Mourinho 
Meneja wa Chelsea Jose Mourinho alishukuru wote aliofanya kazi nao alipokuwa akipokea tuzo kutoka kwa Chama cha Waandishi wa Habari wa Soka wa Uingereza Jumapili.
Mreno huyo alituzwa katika dhifa iliyoandaliwa katika hoteli ya Savoy jijini London saa chache baada ya ushindi wa Chelsea wa 3-1 dhidi ya mabingwa wa Ligi ya Premia Manchester United uwanjani Stamford Bridge ambao uliwapeleka hadi alama mbili nyuma ya viongozi Arsenal.
Kutoka wakati alipojitangaza kuwa "Special One" (Yule wa Kipekee) kabla ya kipindi chake cha kwanza Chelsea, baada ya kushinda Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya akiwa na klabu yake ya zamani Porto, Mourinho ameibuka kuwa kiini kikuu cha vichwa vya habari kwa vyombo vya habari Uingereza.
Lakini kumekuwa na mengi ya kutilia mkazo maneno ya Mourinho, kwani kocha huyo wa miaka 50 aliongoza Chelsea kushinda mataji mawili mfululizo ya Ligi ya Premia 2005 na 2006 mara yake ya kwanza Stamford Bridge kabla ya kukosana na bilionea mmiliki wa klabu hiyo ya London magharibi, Mrusi Roman Abramovich.

Mourinho alienda na akashinda mataji mawili ya ligi Inter Milan, ambapo alishinda pia taji la Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya mara ya pili, na pia akajiunga na miamba wa Uhispania Real Madrid kabla ya kurejea Chelsea kabla ya mwanzo wa msimu huu.
“Bila mapenzi na furaha, singefanya kazi yangu,” alisema Mourinho, aliyeandamana katika karamu hiyo na mkewe na watoto.
Alishukuru sana wote ambao wamesaidia katika ufanisi wake katika soka, akiwemo kocha msifika Mholanzi Louis van Gaal na meneja wa zamani wa Uingereza marehemu Bobby Robson.
"Wasaidizi wangu ni kama ndugu, Frank (Lampard) anawakilisha wachezaji wangu, ambao bila wao singeweza, na Bw van Gaal, Bw Robson, wadosi wangu."
Mourinho alisema maisha mazuri ambayo yeye na familia yake wamejivunia Uingereza yalichangia sana katika kumshawishi kurudi Chelsea.
"Niliketi na mke wangu na familia na kusema ‘ni wapi kuzuri kwetu? Ni wapi tunaweza kuwa na furaha kama familia? Kuwa na furaha kama meneja na pia kujivunia mengi kama familia na kujumuika na jamii?’
"Tuliamua ni Uingereza, baada ya hapo, ili hali iwe njema zaidi ingekuwa ni Chelsea na nilikuwa na bahati kwani milango ilikuwa imefunguliwa,” aliongeza Mourinho ambaye mwanawe wa kiume, Jose Junior, ni kipa stadi anayechipuka.
Mourinho alisema anataka kukaa Chelsea na kufanya mzaha kwamba wakimfuta tena atajiunga na timu nyingine ya Ligi ya Premia, akionyesha mapenzi yake kwa Uingereza.
“Maadili ambayo mnayo kuhusiana na soka na maisha ni ya kupendeza sana,” alifafanua.
“Ninapenda Klabu ya Soka ya Chelsea, ambayo ndiyo klabu pekee ambayo imewahi kunifuta kazi, sisi kama familia ni wenu (hapa) Uingereza.
“Mimi ni wa Chelsea, na Chelsea ni yangu, na natumai kwamba tutakaa hivyo, kwa miaka mingi.”www.skychami.blogspot.com

Post a Comment

Contact Form

Name

Email *

Message *

CHARLES CHAMI. Powered by Blogger.
Javascript DisablePlease Enable Javascript To See All Widget